Saturday, September 7, 2019

SHAIRI : LOLIONDO KWA BABU

Habari natangazia, Kuwapatia uhondo
Nchini Tanzania,   Kijiji cha  Loliondo
Watu viguu na njia, Wanoenda kwa vishindo
Kiongozi wa kanisa, Siku hizi anaganga
Siku imepambazuka, Naamshwa kwa kelele
Najifunga yangu shuka, Kutazama walo mbele
Tayari washazunguka, Kwa Kasisi Ambakile
Kiongozi wa kanisa, Siku hizi anaganga
Miujiza imefika,  Babu yeye keshaota
Wote mloathirika, Anzeni kujikokota
Loliondo mkifika,  Mizizi inatokota
Kiongozi wa kanisa, Siku hizi anaganga
Iwapo una nafasi,  Usiende mhimbili
Ondoa na wasiwasi, Loliondo kuna dili
Dawa bei ni rahisi, Kikombe ni buku mbili
Kiongozi wa kanisa, Siku hizi anaganga
Kashinda madakitari, Walosoma hadi ng’ambo
Magonjwa yote hatari, Yalokuwepo kitambo
Eti mpaka kisukari,  kweli babu ana mambo
Kiongozi wa kanisa, Siku hizi anaganga
Ukimwi unatutisha, Ugonjwa kama adhabu
Waganga wamechemsha, Kutafuta matibabu
Kama mbinu zimekwisha, Kajaribuni kwa babu
Kiongozi wa kanisa, Siku hizi anaganga
Kwa babu kuna vioja, Kabla kutoa tiba
Hutangaza yake hoja, Dawa msije kuiba
Mnapata mara moja, Sio kunywa mkashiba
Kiongozi wa kanisa, Siku hizi anaganga
Wala msifanye pupa,  Walokwenda ni umati
Babu dawa akikupa,  Kunywa  kwa kombe la bati
Usipeleke na chupa, Ukayavunja  masharti
Kiongozi wa kanisa, Siku hizi anaganga
Aponya kila madhara, Hili wengi wanakiri
Pengine ni  biashara, Katumia muhubiri
Kujitoa  ufukara,  Ajipe na utajiri
Kiongozi wa kanisa, Siku hizi anaganga
Mara bibi wa tabora, keshaibuka na yake
Kujiona ndio bora, Na yeye afaidike
Watu kweli ni wakora, Jamani tuwajibike
Kiongozi wa kanisa, Siku hizi anaganga
Sijui kama ya kweli, Msije mkasusia
Mi nahisi utapeli,  Mbuzi ndani ya gunia
Dawa sijaikubali,   Maajabu ya dunia?
Kiongozi wa kanisa, Siku hizi anaganga
Namefika kaditama,  Dawa zinanitatiza
Babu ataniandama,  Malenga kuniapiza
Ninaogopa lawama,  Shairi nimemaliza
Kiongozi wa kanisa, Siku hizi anaganga
HAMZA A. MOHAMMED