Sunday, July 20, 2014

WHAT IS A SPHERE ?

Basic information about spheres

We will start with the basics. A sphere is a set of points in three dimensional space equidistant from a point called the center of the sphere. The distance from the center to the points on the sphere is called the radius of the sphere. Notice that we are talking about the surface of a ball, and not the ball itself. The surface of the earth we live on is a good approximation to a sphere. As you read through this material it would be helpful to have a beach ball about 12'' in diameter with a smooth, solid colored surface, a marking pen, preferably the kind that easily washes off, string, scissors, and a protractor.

Lines and spheres.

If we take an arbitrary line and a sphere in three space, several things can happen. First, the line and the sphere can miss each other. That case is not very interesting. Secondly, the line can intersect the sphere in only one point. In that case the line is tangent to the sphere. The only other thing that can happen is that the line hits the sphere in precisely two points. In particular a line cannot lie in the sphere.
The case which is most interesting is when the line passes through the center of the sphere. In this case the two points of intersection with the sphere are said to be antipodal points. The best known example of antipodal points is the north and south poles on the earth.

Planes, spheres, circles, and great circles.

Next let's look at a plane and a sphere. Again there are several things that can happen. In the uninteresting case the plane and the sphere miss each other. If they do meet each other there are two possibilities. First they can meet in a single point. In this case the plane is tangent to the sphere at the point of intersection. In the other case the sphere and the plane meet in a circle. It is easy to see that the circle of intersection will be largest when the plane passes through the center of the sphere, as it does in the figure to the left. Such a circle is called a great circle. A geographic example of a great circle is the equator. The meridians of longitude form exactly half a great circle. The parallels of latitude are small circles, except for the equator.
Great circles become more important when we realize that the shortest distance between two points on the sphere is along the segment of the great circle joining them. On any surface the curves that minimize the distance between points are called geodesics. Thus lines are the geodesics on the plane, and great circles fill that role on the sphere.
A pretty good approximation to a great circle can be drawn through two points on a beach ball by holding a piece of string tight to the ball at the two points in question. The tightness of the string has the effect of minimizing the length of the string, and therefore closely approximating a geodesic.
We now have the beginnings of a geometry on the sphere. In plane geometry the basic concepts are points and lines. On the sphere we have points, of course, but no lines as such. However, since the great circles are geodesics on the sphere, just as lines are in the plane, we should consider the great circles as replacements for lines. We can then compare the two geometries.
Exercise:
Take your favorite geometry book, and find its list of axioms. Which of the axioms are true for the sphere? If a planar axiom is not literally true on the sphere try to rephrase it so it is true. This exercise cannot be completed at this point. It is one that will continue throughout this material. At this point you should check the axioms of incidence. Remember that a great circle is the intersection of the sphere with a plane that passes through the center of the sphere. Almost every fact we will discover about great circles will follow from that fact.

RATIBA YA MITIHANI KIDATO CHA NNE CSEE ,NOVEMBER 2014.


f RATIBA YA MTIHANI CSEE 2014

TANGAZO LA WATAHINIWA WA KUJITEGEMEA ACSEE 2015.

f TANGAZO ACSEE 2015

MATOKEO YA UALIMU 2014 YATOKA.


f MATOKEO UALIMU 2014

MATOKEO KIDATO CHA SITA ACSEE 2014 YATOKA: BOFYA CHINI -

f MATOKEO ACSEE 2014

USHAIRI NI NINI ?

USHAIRI     NI    NINI ?

Shaaban Robert katika uandishi wa ushairi ameandika Tenzi na mashairi ya kimapokeo.
Tenzi: Ni aina ya mashairi ya kimapokeo wenye sifa zifuatazo:
  • Kimaudhui; Ni utungo wenye maudhui yanayosimulia kwa urefu tukio fulani maalum. Waweza kuwa wasifu wa mtu au jambo la kihistoria. Mfano; S. Robert ameandika utenzi wa vita vya Uhuru, ameeleza kuhusu historia. Pia katika Mapenzi Bora, ameeleza kuhusu sifa za mapenzi bora.
  • Utenzi ni utungo wa pili kati tungo za ushairi zenye beti nyingi. Utungo wa kwanza unaoongoza kuwa na beti nyingi kuliko zote katika ushairi ni Tendi. Lakini hapa tutaangazia tenzi zaidi.
  • Utenzi hauna mizani nyingi aghalabu mizani nane, hauna mshororo bali una nusu mshororo/kipande mstari.
  • Vilevile katika utenzi kipande mstari hakigawiki. Pia katika kipande mshororo kuna vipande vinne kwa kila ubeti. Mistari mitatu ya kwanza huwa na vina vyenye urari na kipande mstari cha mwisho/cha nne huwa na kina tofauti na vipande vya mwanzo. Kina cha mwisho katika mstari wa ubeti hakibadiliki katika beti zote za utenzi.
  • Amri Abead 1954 katika kanuni za kutunga mashairi anakiita kina bahari.
  • Katika utenzi beti huanzia 50-100, lakini wengine wanadai kuwa huanzia beti 100-200
  • Tenzi zote zina sifa ya tarbia
MASHAIRI YA KIMAPOKEO
FANI KATIKA MASHAIRI
lugha; lugha ya kishairi ni lugha ya mjazo, mkato na mnato yenye mpangilio maalum na isiyo na maelezo wala ufafanuzi. Tofauti kabisa na lugha ya kinadhari. Mfano; Riwaya nk.
  • Uteuzi wa sauti, silabi, maneno katika shairi ni wa kipekee usiozingatia sarufi ya lugha.
  • Mpangilio wa maneno katika mshororo huwekwa kwa utaalam zaidi kuliko katika riwaya.
  • Uteuzi wa maneno na semi katika shairi zima kwa kawaida huwa na maana maalum na si suala la kuteuwa tu kiholela holela.
  • Matumizi ya jazanda/picha na taswira. Mfano; mtunzi anaweza kumfananisha mwanamke na ua.
  • Matumizi ya tamathali za semi huwa na maana ambazo hujenga maudhui na kuleta mvuto katika shairi na kufanya kazi ya kishairi iwe ya sanaa zaidi.
  • Matumizi ya lahaja mbalimbali yaani usemaji tofauti tofauti wa lugha moja hutambulisha mkutadha wa mtunzi na muktadha wa walengwa wa lile shairi.
  • Matumizi ya lugha za kigeni – huonesha kiwango cha elimu ya mtunzi na umahiri wake katika lugha. Pia hutambulisha aina ya kazi anayofanya na vilevile, hutambulisha kiwango cha elimu ya watu wanaoandikiwa.
  • Matumizi ya vipengele vya fasihi simulizi kama vile: misemo, nahau, methali, lakabu, nk. hutumika kwa lengo la kuonesha asili ya fasihi andishi kuwa, ni fasihi simulizi na pia huonesha mwingiliano mkubwa wa kimaudhui na kifani katika fasihi simulizi.
MUUNDO WA USHAIRI
Senkoro anasema kuwa, muundo katika kazi ya fasihi ni mpangilio na mtiririko wa kazi hiyo kwa upande wa visa na matukio. Tunachunguza jinsi msanii/mtunzi alivyofuma, alivyosuka, alivyounda na alivyounganisha tukio moja na jingine, wazo moja na jingine, sura moja na nyingine, ubeti mmoja na mwingine, mshororo mmoja na mwingine.
Katika ushairi muundo tunaangalia mpangilio wa beti, mishororo katika ubeti na mtiririko wa visa na matukio katika ubeti na shairi kwa ujumla. Muundo katika ushairi hutazamwa kwa kupimwa idadi ya vina na mizani katika mshororo, idadi ya mishororo katika ubeti na idadi ya beti katika shairi. Tofauti na riwaya au tamthilia ambapo muundo wake huwa wa moja kwa moja/msago, urejeshi/rejea na changamano.
DHANA MUHIMU KATIKA SHAIRI.
  • Mshororo – ni mstari wa ushairi katika ubeti. Kwa mujibu wa wanamapokeo mshororo si lazima uwe na maana. Lakini wanausasa/mamboleo wanadai kuwa kila mshororo katika ushairi lazima uwe na maana. Mshororo huweza kuwa na kipande; kimoja, viwili, vitatu au zaidi.
Vipande katika ushairi ni sehemu ya mshororo au mstari wa ushairi katika ubeti.
  • Vibwagizo au kituo – huu ni mshororo wa mwisho katika ubeti ambao kwa kawaida hujirudia rudia. Pia huweza kuwa na majina tofauti tofauti kulingana na kinavyotumika. Huweza kuitwa kibwagizo kiini au bahari – yaani kile kinachojirudia katika kila ubeti.
Pia kuna kibwagizo kawaida – hiki hubadilika badilika katika kila ubeti.
Kwa ujumla kibwagizo husaidia sana kushadidia dhamira kuu au wazo kuu katika shairi, na pia husaidia kujenga takriri katika shairi kama kipengele cha matumizi ya lugha katika fani.
  • Ubeti – ni fungu la mistari/mishororo iliyopangwa pamoja katika shairi na inayoleta maana kamili inayojitosheleza. Beti nyingi katika mashairi hutumia tarbia/mistari minne. Pia beti huweza kuanzia mstari mmoja na kuendelea.
Majina ya mishororo katika ubeti:
  • Mshororo wa kwanza huitwa mwanzo
  • Mshororo wa pili huitwa mlato
  • Mshororo wa tatu huitwa mleo
  • Mshororo wa nne huitwa kimalizio, kibwagizo, kituo, mkarara, kipokeo.
Shairi huweza kuundwa na kipande mstari yaani ubeti wenye kipande mstari.
  • Kipande mstari cha kwanza huitwa ukwapi
  • Kipande mstari cha pili huitwa utao
  • Kipande mstari cha tatu huitwa mwanda.
  • Mizani – Idadi ya silabi katika mshororo. Hutumika kama kipimo cha ushairi kwani huhesabiwa kwa uwiano. Mashairi ya kimapokeo yana mizani 16, katika ukwapi 8 na katika utao 8 jumla 16
  • Urari – ulingano/uwiano wa vina na mizani katika mashairi. Mashairi ya kimapokeo urari ni msingi wa utunzi. Urari katika ushairi/mashairi husaidia kuimbika kwa shairi ambayo ndio sifa mahususi ya mashairi ya kimapokeo.
  • Vina – ni silabi zenye milio inayofanana, ni silabi za kati mwishoni mwa kipande mshororo na silabi za mwisho katika mshororo.
·    Vina vya kati vinaweza kuwa vina vya ukwapi na utao katika shairi lenye vipande mstari vitatu.
·   Wakati katika shairi lenye vipande mstari viwili vina vya kati huwa ukwapi. Pia katika shairi lenye kipande mstari kimoja kina cha kati huwa hakuna.
·       Shairi lenye vipande mstari vitatu; mfano, ………., …………., …………., kina cha mwisho ni mwanda.
·     Shairi lenye vipande mstari viwili, mfano; ……..…….., …………..….., kina cha mwisho ni utao.
·   Shairi lenye kipande mstari kimoja kina cha kati ni ukwapi. mfano, …………….,
DHIMA YA VINA
  • Vina huleta mvuto katika kughana shairi.
  • Husisitiza maudhui katika shairi
  • Vina vya shairi hutumika kumalizia kipande au mshororo mzima wa shairi.
  • Husaidia kuhifadhi au kushika kichwani/kukariri kwa urahisi kutokana na kujirudia rudia.
MTINDO KATIKA USHAIRI
Ni mbinu au namna anayotumia mtunzi katika kuandika kazi yake. Mtindo pia ni mbinu au namna na vilevile ni tabia ya utungaji wa mashairi unaompambanua mtunzi mmoja na mwingine.
  • Katika mtindo tunaangalia, kwa nini mtunzi ametumia lahaja au maneno magumu. Pia tunaangalia tamathali za semi, methali, nahau nk.
  • Vilevile tunaangalia mpangilio wa mishororo katika ubeti, je ni vipande vitatu au viwili au vinne.
  • Pia tunaangali mwandishi ametumiaje takriri katika shairi, je ni takriri sauti, takriri neno nk.
  • Vilevile tunaangalia mwandishi ameunda vipi shairi lake; ameanza vipi na amemalizia vipi shairi lake. Maswali haya yakijibiwa ndipo tunaweza kujua mtindo wa mshairi.
  • Pamoja na hayo, pia kuna mbinu ya kutumia michoro/vielelezo nk. mfano katika kitabu cha Insha na Mashairi.
  • Mbinu nyingine katika mtindo ni ile ya kuanza na aya za mashairi kwa kutumia herufi kubwa katika neno la kwanza.
  • Pia kuna mbinu ya kikufu; yaani kuanza na kina cha mwisho cha ubeti uliotangulia.
  • Vilevile kuna mbinu ya pindu; yaani neno la mwisho au kipande cha mwisho huanza katika mshororo wa pili. Mbinu pindu inaunganisha mshororo.
  • S. Robert pia ametumia mbinu ya kuchanganya kazi mbili au zaidi katika diwani moja “two in one”. Mfano, Tenzi, Insha na Shairi. Katika riwaya ya “Maisha yangu na Baada ya Miaka Hamsini
  • Licha ya hayo, pia tunaangalia mbinu zinazojenga maana na matumizi ya lugha. Mfano; mashairi ya S. Robert ametumia mbinu ya kidatu, yaani kufupisha mshororo mmoja au zaidi katika kila beti. Anaweza kufupisha mshororo, kipande mshororo au neno. Mfano, katika Insha na Mashairi.
  • Vilevile S. Robert ametumia mbinu ya kufasili maneno magumu/msamiati mgumu.
MUKTADHA
  • Muktadha katika kazi ya fasihi hurejelea mahali na wakati mtunzi anapoandika/alipoandika kazi yake ya fasihi. Mazingira huweza kuwa ya kihistoria, kijiografia, kijamii nk.
  • Pia katika muktadha tunaangalia watu waliozungumziwa katika muktadha huo,
  • Vilevile mazingira ya kiutendaji – hapa tunaangalia namna gani mambo yametendeka.
  • Muktadha husaidia katika kujenga wahusika au mtunzi mwenyewe. Pia husaidia kujenga lugha.
  • Pia katika uhakiki wowote usiozingatia muktadha wa kazi husika kwa kawaida hupotosha kazi husika katika upande wa maudhui au fani.

TAMTHILIA NI NINI ?

TAMTHILIA

UANDISHI WA TAMTHILIA
Tamthilia ni nini?
  • Tamthilia ni utanzu ambao hutegemea mazungumzo na uigizaji ili kuwasilisha ujumbe wake. Huu ni utanzu ambao huandikwa kwa mtindo wa mazungumzo ya wahusika (Wamitila, 2007).
  • Nkwera (h.t) anaelezea kuwa tamthilia ni: Tamthilia ni mchezo wa kuigiza au utungo wa kisanaa ambao huweka wazo fulani katika matendo na mazungumzo (Nkwera, h.t)
AINA ZA TAMTHILIA
  • Kwa mujibu wa Aristotle, kuna aina mbili za tamthilia. Aina ya kwanza ni tanzia na nyingine ni ramsa.
  • Tanzia ni nini?
Tanzia ni kinyume cha ramsa kwa maana kuwa hutumika kuonesha kuanguka na kushindwa kwa mhusika maarufu, mbabe, au shujaa atokaye katika tabaka la juu yaani mtu wa nasaba bora (Mutembei, 2005 katika mihadhara ya SW 234).
Kama ilivyo kwa ramsa, tanzia ilianzia katika miviga ya kidini, katika sherehe ya kumhusu Dionisius. Wachezaji na Waigizaji walivalia na kuonekana kama mbuzi wakiimba nyimbo zilizohusu anguko la shujaa (Mutembei, 2005 katika mihadhara ya SW 234).
ARISTOTLE TANZIA ANAONA KUWA; Tanzia ni usanii uoneshao anguko la mtu ambaye kimsingi ni mwema, shujaa au mbabe kutokana na kosa la kufisha au kutokana na uamuzi mbaya ambao matokeo yake ni mateso (Mutembei, 2005 katika mihadhara ya SW 234).
Jambo hili linapompata shujaa huyo, jamii nzima huingia katika woga na kuhangaika kwa hali ya juu, kwani kiongozi wao yumo katika mateso na ni uchuro wa kufisha jamii kama hatua madhubuti hazitachukuliwa (Mutembei, 2005 katika mihadhara ya SW 234)
MISINGI YA UTOKEAJI WA TANZIA:
Kwa mujibu wa Mutembei, (kashatajwa) katika mihadhara ya SW 234 anasema kuwa, misingi ya utokeajiwa tanzia inapaswa izingatie yafuatayo:
  • Iwe na uwezo wa kuamsha hisia za woga na huruma miongoni mwa hadhira.
  • Shujaa au mbabe apataye mkasa ni lazima awe mwema na mwenye kuvutia kwa sura/umbo zuri.
  • Watazamaji huonesha kuumia, husikitika nk. kadri mtu anavyoonekana ni mwema au mzuri wa umbo lake kama ilivyokuwa kwa mhusika wa Second Chance – Salvado Solenza.
  •  Katika Tanzia, anguko la shujaa huja kutokana na ama uamuzi wake mbaya au kosa lake mwenyewe. Aristotle: alisema kuwa, hakuna kosa la bahati mbaya. Kila mkasa wa kufisha ni matokeo ya maamuzi mabaya, au kosa fulani.
ISTILAHI KATIKA TANZIA:
HUBRISI- Dhambi yenyewe. Kitendo chenyewe akitendacho shujaa ambacho humwingiza katika hamartia.
ANAGNORISIS- Utambuzi wa ndani. Ni ile saa ambapo shujaa hupata utambuzi wa ndani katika akili ya shujaa  ambao humjulisha kuwa kakosea na tayari kesha jitumbukiza katika anguko kuu. (Mutembei, 2005 katika mihadhara ya SW 234)
PERIPATEA-Matendo muhimu ambayo humtoa shujaa katika hali iliyoonekana kuwa afadhali kumdidimiza  katika hali mbaya kabisa. (Mutembei, 2005 katika mihadhara ya SW 234) 
NEMESIS- Adhabu ambayo haina budi kuwapo kutokana na matendo ya Hubrisi (Mutembei, 2005 katika mihadhara ya SW 234).
  • Ramsa ni nini?
Ni aina ya tamthilia ambayo hadhira inapoangalia isiogope au kupata uchungu bali icheke kwa kumkejeli mhusika kutokana na matendo yasiyofurahisha katika jamii. Mhusika anatakiwa amfanye matendo au tabia ambazo ni kinyume na maadili ya jamii, ili yanapomkuta masahibu – hadhira Imcheke kwa upumbavu na uzembe wake. Mfano mzuri ni mikasa inayoonesha baadhi ya wanandoa kutokuwa waaminifu katika ndoa zao – wanapokumbwa na fumanizi na kuumbuka, hadhira itamcheka mhusika kwa kuwa ayafanyayo hayakubaliki katika maadili. Vilevile aina hii ya tamthilia huishia na mwisho wa kufurahisha.
SHUJAA WA KI-RAMSA
Kwa mujibu wa (Mutembei, 2005 katika mihadhara ya SW 234), shujaa wa kiramsa ni mtu mwenye sifa zifuatazo:
  • Sio lazima awe mtu maarufu au Mbabe/Shujaa anaweza kuwa ni kichaa au mwendawazimu fulani ambaye yuko katika jamii
  • Mtu ambaye katika jamii huwa duni, na matendo yake ni ya kiucheshi-ucheshi, ila historia humlea na kumkuza hata akatokea kuwa “fulani” – akaishi raha mustarehe.
  • Mhusika ambaye akifanikiwa kila mtu atafurahia na baada ya igizo atakuwa ameridhishwa na mwisho huo mzuri wa kuishi raha mustarehe.
UHUSIKA WA WAHUSIKA WA KI-RAMSA
  • Ramsa huwahusu watu wa kawaida ambao wana kipato cha kati na chini kama vile: washona viatu, wauza mitumba, wakata nyama, wachoma mishikaki, wanafunzi, walimu, wasukuma mikokoteni, n.k. Ramsa haihusu  watu wa juu ambao ni kama vile: wafalme, malkia, viongozi, watu wote wa nasaba BORA (Mutembei, 2005 katika mihadhara ya SW 234)
  • Ramsa huhusika na mambo ya kawaida yanayowahusu watu wa kawaida katika maisha ya kila siku (Mutembei, 2005 katika mihadhara ya SW 234). Mambo kama: Kupata rafiki mpya (au Kumrudisha wa zamani) au kupata kazi au kupanda cheo kwa mfano akina Mkwere kwenye Mizengwe kila Jumapili saa tatu usiku, kituo cha ITV.
DHAMIRA ZA KI-RAMSA
Ramsa huhusika na mambo ya kawaida yanayowahusu watu wa kawaida katika maisha ya kila siku (Mutembei, 2005 katika mihadhara ya SW 234). Mambo kama: Kupata rafiki mpya (au Kumrudisha wa zamani) au kupata kazi au kupanda cheo kwa mfano akina Mkwere kwenye Mizengwe/Ucheshi kila Jumapili saa tatu usiku, kituo cha ITV.
AINA ZA RAMSA:
UTANI/VICHEKESHO (farce)
Huonekana ni upuuzi, mambo hugeuzwa kinyume. Sura za wahusika hubadilishwa - kama vinyago. Lengo ni kuchekesha na ndimo maana yake hupatikana. Mfano tunaweza kuziweka kazi za Mzee Majuto katika aina hii japo sio sifa zote za utani zinajitokeza katika kazi zao
MAHABA/MAPENZI (romance)
Wapendanao, huwekewa vikwazo (pesa, kabila, hadhi) lakini hatimaye hushinda vikwazo hivyo. Hupendana na kuoana (Mutembei, 2005 katika mihadhara ya SW 234). Tazama kazi nyingi za filamu hapa nyumbani zinaangukia katika kundi hili; mfano ni Sandra, Johari, Sikitiko langu The Game of Love kwa kuzitaja kwa uchache.
TASHTITI/ DHIHAKA- (satire) ni zile kazi zinazolenga kuwasilisha dhihaka kwa viongozi, siasa, au dini (Mutembei, 2005 katika mihadhara ya SW 234). Kwa mfano zamani Ze Comedy ilipokuwa ikirusha vipindi vyake kupitia East Africa Television (EATV); kwa sasa wanatambulikana kama Origino Komedí ila wamepwaya katika uwasilishaji wao – sio kama zamani. Nadhani kuna udhibiti ndani yake.
  • Pia tashititi hizi huhusisha kuakisi yafanywayo na wahalifu, matapeli, wanafiki, wala rushwa, wafanya magendo, waongo n.k. Mfano ni Bongo Darisalaam kilichokuwa kinachorushwa na TBC1.
  • Mhusika mkuu (ambaye ni Kiongozi) huwa na sifa hizo hapo juu na anadhihakiwa ili aache rushwa, uhalifu, utapeli, nk.
  • Ramsa hizi ni kama – njia ya walala hoi kutoa malalamiko yao kwa viongozi wao kwa mfano angalia kazi za Futuhi inayorushwa na Kituo cha Utangazaji cha Star Tv kila Alhamisi usiku saa tatu.
VIPENGELE VYA TAMTHILIA
  • Vipengele vya kifani katika tamthilia ni pamoja na: wahusika, mtindo, muundo, mandhari, jina la kazi, na matumizi ya lugha.
VIPENGELE VYA SANAA ZA MAONESHO
Vipengele vya sanaa za maonesho kwa mujibu wa Aristotle na Semzaba ni hivi vifuatavyo: uhusika na wahusika, maudhui, msuko wa matukio, uteuzi wa lugha, kionwa, na muziki.
Vipengele hivi vya sanaa za maonesho vimejadiliwa katika kitini cha Uandishi wa Kubuni kwa Kiswahili Nadharia na Vitendo kilichoandikwa na Mahenge, E. Soma vipengele hivyo na uvitumie katika kuhakiki kazi za sanaa za maonesho.
MAUDHUI YA TAMTHILIA
  • Maudhui ya tamthilia yanagusia vipengele vya: migogoro, ujumbe, falsafa, mtazamo, msimamo, na dhamira.
  • Matumizi ya tamthilia ni pamoja na: kuelimisha jamii; (katika masuala mbalimbali kama vile: uchumi, siasa, maadili, nk.) kuburudisha jamii, kuonya na kukosoa jamii, kukuza lugha, kurithisha amali za jamii (mila na desturi za jamii husika), nk.

FASIHI SIMULIZI TANZU NA VIPERA VYAKE.

FASIHI    SIMULIZI  VIPERA   NA   TANZU   ZAKE.

Kwa mujibu wa Mulokozi katika Mulika namba 21(1989). Pamoja na kwamba Fasihi ni kongwe lakini kitaaluma bado ni changa kwa sababu ilianza kuchungunzwa hivi karibuni. Hivyo imepelekea kutokuwepo kwa nadharia, marejeo, wala istilahi zenye kutosheleza mahitaji ya taaluma hiyo. Tatizo hili linadhihirika pale tunapoangalia kazi za wataalamu mbalimbali kuhusu tanzu za Fasihi Simulizi. Kwa upande wa nadharia kitabu pekee kinachozijadili tanzu za Fasihi Simulizi kwa urefu ni kitabu cha Ruth Fennegan kinachoitwa Oral Literature in Africa (1970). Kwa upande wa Kiswahili hakuna kitabu kinachojadili uwanja wa tanzu za Fasihi Simulizi. Badala yake kunamiongozo michache kwa ajili ya shule za sekondari kama vile Balisidya, N (1975) na Taasisi ya Elimu (1987)
Mulika namba 21 ni jarida la kitaaluma linalotoa fursa kwa wataalamu, waalimu na wanafunzi katika kujadili mada mbalimbali za kiswahili. Jarida hili lililoandikwa mwaka 1989 ndani yake kuna makala ya Fasihi Simulizi inayohusu tanzu za Fasihi Simulizi na vipera vyake iliyoandikwa na M.M.Mulokozi.

Hivyo basi kutokana na kukosekana kwa nadharia zinazoongoza ugawaji wa tanzu za Fasihi Simulizi ya Kiswahili wataalamu wengi wamekuwa wakitumia vigezo mbalimbali ambavyo ni maudhui, fani, matukio, idadi ya waimbaji, vifaa vinavyotumika na namna ya uimbaji.
Fasihisi Simulizi imejadiliwa na wataalamu mbalimbali miongoni mwa waalamu hao ni M.M.Mulokozi (1996) anasema Fasihi Simulizi ni fasihi inayotungwa au kubuniwa kichwani na kuwasilishwa kwa hadhira kwa njia ya mdomo na vitendo bila kutumia maandishi.
TUKI (2004) Fasihi Simulizi ni kazi ya fasihi inayohifadhiwa na kurithishwa kutoka kizazi kimoja hadi kingine kwa njia ya mdomo kama vile; hadithi, ngoma na vitendawili. 
Hivyo basi Fasihi Simulizi ni fasihi inayotokana na maneno ambayo huzungumzwa, hutolewa au kuimbwa ambapo mtungaji na mwasilishaji hutumia sanaa.
Tanzu ni istilahi inayotumiwa kuelezea au kurejelea aina ya kazi mbalimbali za kifasihi. Inawezekana utanzu mkuu kuwa na vitanzu vingine mbalimbali kwa mfano, tanzu kuu za kifasihi ni Riwaya, Tamthilia, Shahiri, Novela, Insha na Hadithi (Wamitila (2003).
Vipera ni dhana inayotumiwa kuelezea vijitanzu katika fasihi hasa fasihi simulizi. Mfano: semi methali, mafumbo, vitendawili nakadhalika. (Wamitila 2003)
M.M.Mulokozi katika makala yake ya tanzu za Fasihi Simulizi iliyo katika jarida la Muulika namba 21(1989) amezigawa tanzu na vipera vya Fasihi Simulizi kwa kutumia vigezo viwili ambavyo ni,kigezo cha kwanza ni umbile na tabia ya kazi inayohusika na kigezo cha pili ni muktadha na namna ya uwasilishaji wake kwa hadhira.
Umbile na tabia ya kazi inayohusika: katika kigezo hiki Mulokozi ameangalia vipengele vya ndani vinavyoiumba sanaa hiyo na kuipa muelekeo au mwenendo. Baadhi ya vipengele hivyo vya ndani ni namna lugha inavyotumika (kishahiri, kinathari, kimafumbo, kiwimbo na kighani), muundo wa fani hiyo na wahusika.
Kwa upande wa muktadha na namna ya uwasilishaji amezingatia kuwa, Fasihi Simulizi ni tukio hivyo huambatana na muingiliano wa mambo matatu ambayo ni muktadha, watu na mahali. Mwingiliano huu ndio unaotupa muktadha na muktadha ndio unaoamua fani fulani ya Fasihi Simulizi ichukue umbo lipi, iwasilishwe vipi kwa hadhira, kwenye wakati na mahali hapo. Hivyo hadithi inaweza kugeuzwa wimbo, utendi unaweza kuwa hadithi na wimbo unaweza kugeuzwa ghani au usemi kutegemea muktadha unaohusika (Mulokozi 1989).
Kwa hiyo kwa kutumia vigezo hivi, Mulokozi amezigawa tanzu na vipera vya Fasihi Simulizi kama ifuatavyo;
Masimulizi; hii ni tanzu ya Fasihi Simulizi yenye kusimulia habari fulani. Katika kugawa utanzu huu vigezo vilivyotumika ni pamoja na kigezo cha lugha ambapo lugha inayotumika katika masimulizi ni ya kinathari. Pia kigezo kingine ni kigezo cha muundo, mara nyingi masimulizi huwa na muundo unaojitofautisha na tanzu nyingine kama vile ushairi. Katika masimulizi muundo wake mara nyingi huwa wa moja kwa moja yaani mtiririko wa visa na matukio. Vilevile kigezo kingine ni kigezo cha wahusika ambapo katika kigezo hiki huhusisha wahusika wa pande mbili ambao ni mtendaji na watendwaji. Pia kigezo kingine ni kigezo cha namna ya uwasilishaji. Katika uwasilishwaji huwasilishwa na msimuliaji mbele ya hadhira. Kigezo kingine ni kigezo cha mandhari ambayo huwa maaluma kama vile chini ya mti mkubwa na uwanjani. Masimulizi pia hufanyika katika muda maalum. Mfano, baada ya kazi.
Masimulizi yamegawanyika katika tanzu kuu mbili ambazo ni tanzu za kihadithi (za kubuni) na tanzu za kisalua (kihisitoria). Tanzu za kihadithi zina kipera kimoja ambacho ni ngano. Ngano (vigano/hurafa), hizi ni hadithi za kimapokeo zitumiazo wahusika kama wanyama, miti na watu kuelezea na kuonya kuhusu maisha.  Vigezo vilivyotumika katika kugawa ngano ni kigezo cha lugha ambayo ni lugha ya kinathari, kigezo cha dhima ambacho huelezea au kuonya kuhusu maisha na kufurahisha. Kigezo kingine kilichotumika ni kigezo cha wahusika ambao ni wanyama, miti na watu. Kipera hiki cha ngano kinajumuisha vijipera vifuatavyo ambavyo ni istiara, mbazi na kisa.
Istiara; hii ni hadithi ambayo maana yake ya wazi inawakilisha maana nyingine iliyofichika. Vigezo vilivyotumika katika kugawa kipera hiki ni kigezo cha lugha ambayo ni lugha ya mafumbo.
Mbazi; hii ni hadithi fupi yenye mafunzo itolewayo kama kielelezo wakati wa maongezi au kumkanya mtu. Kigezo kilichotumika katika kugawa kipera hiki ni kigezo cha dhima.
Kisa; hii ni hadithi fupi ya kufurahisha kuhusu tukio la kweli. Kigezo kilichotumika ni kigezo cha kidhima.
Utanzu mwingine wa masimulizi ni utanzu wa kisalua. Utanzu huu umegawanyika katika vipera vifuatavyo ambavyo ni visakale, mapisi, tarihi, kumbukumbu na visasili.
Visakale; haya ni masimulizi ya mapokeo juu ya wahenga au mashujaa wa kabila au taifa yenye kuchanganya chuku na historia (kama hadithi ya Liyongo). Vigezo vilivyuotumika hapa ni kigezo cha wahusika ambao wapo katika historia yaani mashujaa fulani. Kigezo kingine ni fani ya ubunifu.
Mapisi; haya ni maelezo ya kihistoria bila kutia mambo ya kubuni. Hapa pia kigezo kilichotumika ni kigezo cha dhima ambacho huelezea mambo ya kihistoria yaliyo ya kweli.
Tarihi; haya ni maelezo au jedwali la matukio muhimu na tarehe zake. Kigezo kilichotumika hapa ni kigezo cha kidhima ambacho ni kuelezea matukio muhimu na tarehe zake. Pia kigezo kingine ni namna ya uwasilishaji ambapo huwasilishwa kwa kutumia jedwali na lugha yake huwa katika maandishi.
Kumbukumbu; haya ni maelezo ya matukio muhimu yanayomuhusu mtu binafsi au jamii ya watu. Hapa kimetumika kigezo cha fani, ambayo ni fani za wasifu na tawasifu. Pia kigezo kingine ni kigezo cha wahusika ambao ni watu.
Visasili; hiki ni kipera kinachofungamana na imani za dini na mizungu ya kajamii pia hizi ni hadithi za kale zenye kuwakilisha imani na mtazamo wa jamii inayohusika kuhusu asili ya ulimwengu na maisha yao. Kigezo kilichotumika ni kigezo cha kidhima ambacho huelezea shabaha ya maisha.
Utanzu mwingine wa Fasihi Simulizi ni utanzu wa Semi. Semi ni tungo au kauli fupi fupi za kisanaa zenye kubeba maana au mafunzo. Kigezo kilichotumika katika kugawa utanzu huu ni kigezo cha lugha ambayo ni lugha ya mkato. Kigezo kingine ni kigezo cha kidhima ambacho ni kufunza.
Utanzu huu umegawanyika katika vipera vifuatavyo ambavyo ni methali, vitendawili, misimu, mafumbo na lakabu.
Methali ni semi fupi fupi zenye kueleza kwa mukhtasari fikra au mafunzo mazito yaliyotokana na uzoefu wa kijamii. Vigezo vilivyotumika katika kipera hiki ni kigezo cha lugha ambayo ni lugha ya mafumbo. Vilevile kimetumika kigezo cha muundo ambapo methali huundwa na muundo wa pande mbili ambazo hutegemeana.
Vitendawili; huu ni usemi uliofumbwa ambao hutolewa kwa hadhira ili ufumbuliwe. Vigezo vilivyotumika ni kigezo cha lugha. Hapa lugha inayotumika ni lugha ya kimafumbo.
Misimu; ni semi za muda na mahali maalum ambazo huzuka na kutoweka kutegemea mazingira maalum. Hivyo vigezo vilivyotumika katika kugawa kipera hiki ni kigezo cha muktadha yaani hutokea wakati maalum na mazingira maalum.
Mafumbo; ni semi za maonyo au mawaidha ambazo maana zake za ndani zimefichika. Kigezo kilichotumika ni kigezo cha kidhima ambacho ni kuonya pamoja na kigezo cha lugha ambayo ni lugha ya mafumbo.
Lakabu; haya ni majina ya kupanga ambayo baadhi ya watu hupewa au hujipatia kutokana na sifa zao za kimwili, kinasaba, kitabia au kimatendo. Kigezo kilicho tumika katika kipera hiki ni kigezo cha lugha ambayo lugha iliyotumika ni lugha kificho yaani maana yake hufichwa.
Utanzu mwingine wa Fasihi Simulizi ni ushairi. Huu ni utanzu wa fasihi simulizi unaowasilishwa kwa hadhira kwa njia ya uimbaji au ughani badala ya usemaji wa kawaida. Vigezo vilivyotumika katika kugawa utanzu huu ni kigezo cha lugha ambayo ni lugha ya kishairi. Pia kimetumika kigezo cha fani ambapo fani inayotumika ni wizani, lugha ya mkato, lugha ya mafumbo na uimbaji au ughani.
Katika utanzu huu kuna vipera viwili ambavyo ni nyimbo na maghani;
Nyimbo ni kila kinachoimbwa. Vigezo vilivyotumika katika kipera hiki cha ushairi ni kigezo cha fani ambapo huangalia muziki wa sauti ya muimbaji au waimbaji, muziki wa ala (kama ipo), matini au maneno yanayoimbwa. Pia kuna kigezo cha muktadha ambacho huzingatia hadhira inayoimbiwa na muktadha unaofungamana na wimbo huo, kwa mfano sherehe, ibada, kilio nakadhalika. Kwa vigezo hivi utanzu wa nyimbo umegawanyika katika vijipera vifuatavyo ambavyo ni, tumbuizo, bembea, kongozi, nyimbo za dini, wawe, tenzi, tendi, mbolezi, kimai, nyiso, nyimbo za vita, nyimbo za uwindaji, nyimbo za taifa, nyimbo za watoto na nyimbo za kazi.
Tumbuizo; hizi ni nyimbo za furaha ziimbwazo kuwafurahisha watu kwenye matukio mbalimbali kama vile ngomani au harusini. Vigezo vilivyotumika hapa ni kigezo cha kidhima ambacho hulenga kuwafurahisha watu, pia kigezo kingine ni kigezo cha kimuktadha ambapo huwasilishwa katika matukio yanayoendana na dhima ya kufurahisha.
Bembea; hizi ni nyimbo za kubembeleza watoto. Kigezo kilichotumika hapa ni kigezo cha kidhima ambapo hulenga kubembeleza watoto.
Kongozi; hizi ni nyimbo za kuaga mwaka. Vigezo vilivyotumika hapa ni kigezo cha kidhima ambapo dhima yake ni kuaga mwaka na kigezo cha kimuktadha ambapo muktadha wake ni muktadha maalum yaani huimbwa mwishoni mwa mwaka.
Nyimbo za dini; hizi ni nyimbo zinazoimbwa kwa lengo la kumsifu Mungu au miungu. Vigezo vilivyotumika ni kigezo cha kidhima ambapo dhima yake ni kumsifu Mungu au miungu, pia kimetumika kigezo cha kimuktadha ambapo huimbwa katika muktadha wa kidini.
Wawe; hizi ni nyimbo za kilimo. Vigezo vilivyotumika ni kigezo cha kimuktadha ambapo huuimbwa wakati wa kulima, pia kigezo cha kidhima kimetumika ambapo dhima yake ni kuchapusha kazi.
Tenzi; hizi ni nyimbo ndefu za kimasimulizi au mawaidha. Kigezo kilichotumika ni kigezo cha kifani ambapo fani yake ni masimulizi au mawaidha.
Tendi; hizi ni nyimbo ndefu za masimulizi juu ya matendo ya mashujaa. Vigezo vilivyotumika hapa ni kigezo cha kifani ambapo wahusika wa tendi ni watu wenye historia za matendo ya kishujaa, pia kigezo cha lugha kimetumika ambapo lugha yake ni ya kinathari.
Mbolezi; hizi ni nyimbo za kilio au maombolezo. Vigezo vilivyotumika katika kugawa kipera hiki ni kigezo cha kimuktadha ambapo huwasilishwa katika muktadha wa maombolezo au kilioni/msibani, pia kimetumika kigezo cha kidhima ambapo dhima yake ni kuomboleza.
Kimai; hizi ni nyimbo zihusuzo shughuli za baharini. Vigezo vilivyotumika hapa ni kigezo cha kidhima ambapo dhima yake ni kuchapusha kazi. Vilevile katika kigezo cha kimuktadha kimai huwasilishwa katika mazingira ya baharini.
Nyiso; hizi ni nyimbo za jandoni. Vigezo vilivyotumika ni kigezo cha kidhima ambapo dhima yake ni kutoa mafunzo kwa vijana kuhusu maisha ya utu uzima. Kigezo kingine ni kigezo cha kimuktadha ambapo nyiso huwasilishwa katika mazingira maalumu, kama vile porini nakadhalika.
Nyimbo za vita; hizi ni nyimbo ziimbwazo na askari wakati wa vita. Vigezo vilivyotumika katika kugawa kipera hiki ni kigezo cha kimuktadha ambapo muktadha wake huwa ni wakati wa vita, na kigezo kingine ni kigezo cha wahusika au waimbaji ambapo waimbaji wake huwa ni maaskari.
Nyimbo za watoto, hizi ni nyimbo waimbazo watoto wakati wa michezo yao. Vigezo vilivyotumika ni pamoja na kigezo cha kimuktadha ambapo huwasilishwa wakati wa michezo ya watoto. Kigezo kingine ni kigezo cha wahusika au waimbaji ambapo waimbaji wake huwa ni watoto.
Nyimbo za uwindaji; hizi ni nyimbo ambazo huimbwa na makundi ya wawindaji wakati wa shughuli au sherehe zao. Vigezo vilivyotumika hapa ni kigezo cha wahusika au waimbaji ambapo huimbwa na wawindaji na kigezo kingine ni kigezo cha kimuktadha ambapo huwasilishwa wakati wa shughuli au sherehe za uwindaji.
Nyimbo za Taifa; hizi ni nyimbo za kisifia Taifa au kabila. Kigezo kilichotumika hapa ni kigezo cha kidhima ambapo dhima yake ni kusifia Taifa au kabila.
Nyimbo za kazi; hizi ni nyimbo zinazoimbwa katika shughuli mbalimbali kama vile, kulima, kutwanga, kusuka, uvuvi, uashi, useremala na kadhalika. Vigezo vilivyotumika hapa ni kigezo cha muktadha wa uwasilishaji ambapo huwasilishwa kulingana na shughali maalumu. Pia kigezo kingine ni kigezo cha kidhima ambapo dhima ya nyimbo za kazi ni kuchapusha kazi.                
Maghani; hiki ni kipera cha ushairi kinachotolewa kwa kalima badala ya kuimbwa. Kwa mujibu wa Wamitila (2003) maghani ni istilahi inayotumiwa kuelezea aina ya ushairi ambao hutolewa kwa kalima au maneno badala ya kuimbwa. Vigezo vilivyotumika katika kugawa utanzu huu ni lugha ambayo ni lugha ya kishairi. Pia ametumia kigezo cha wahusika ambapo wahusika wakuu ni binadamu. Hivyo vigezo hivi ndivyo vilivyopelekea utanzu huu kuwekwa kwenye utanzu wa ushairi.
Kipera hiki kina vijipera vitatu ambavyo ni maghani ya kawaida, sifo na maghani masimulizi. Maghani ya kawaida ni kundi ambalo tunaweza kuingiza fani mbalimbali za ushahiri simulizi kama vile ushairi wa mapenzi, siasa, maombolezo, kazi, dini ilimradi unaghanwa katika namna ya uwasilishwaji wake.
Sifo; hizi ni tungo za kusifu ambazo husifu watu, wanyama na mimea. Baadhi ya sifo huwa zinakashifu au kukejeli. Vigezo vilivyotumika katika kugawa kipera hiki ni kigezo cha wahusika, wahusika wake wakuu ni binadamu wanyama au mimea. Kigezo kingine ni muktadha ambao huelezea matukio yaliyopita au yaliyopo. Sifo huwa na tanzu muhimu kama vile vivugo (majigambo), pembezi na tondozi.
Kivugo; hili ni ghani la kujisifia, hutungwa na kughanwa na muhusika mwenyewe. Vigezo vilivyotumika katika kugawa kijipera hiki cha sifo ni lugha, katika lugha zimetumika mbinu kama vile sitiari, mkato, vidokezo, ishara, takriri na vina. Kigezo kingine ni kigezo cha wahusika ambapo wahusika wake wakuu ni binadamu pia kimetumika kigezo cha muktadha ambapo muktadha wake hufungamana na tukio maalum katika maisha ya muhusika, mfano vitani. Vilevile katika kigezo cha uwasilishaji huweza kuwa na masimulizi ndani yake. Muundo wake hutegemea shabaha za mtunzi na jadi ya utunzi anayoiwakilisha hakiandikwi na kutungwa papo kwa papo.
Tondozi; hizi ni tungo za kusifu watu, wanyama au vitu. (Pembezi pia ni aina ya tondozi ambayo imekusudiwa watu wa aina fulani tu). Vigezo vilivyotumika katika kugawa kipera hiki ni kigezo cha wahusika ambao ni wanyama na mimea. Mfano wa wanyama ni kama vile Simba. Kigezo kingine ni lugha ambayo ni lugha ya kishairi.  
Ghani masimulizi: hizi ni ghani ambazo hutambwa ili kusimulia hadithi, historia au tukio fulani. Vigezo vilivyotumika kugawa kipera hiki ni pamoja na kigezo cha lugha, lugha inayotumika katika kijipera hiki ni lugha ya kishairi na fani iliyotumika ni kusimulia hadithi/tukio kwa kirefu. Vile vile kuna kigezo cha namna ya uwasilishaji huambatana na ala za muziki mfano zeze na marimba.
Ghani masimulizi ina vipera vinne ambavyo ni rara, ngano, sifo na tendi.
Rara ni hadithi fupi nyepesi ya kishairi yenye visa vya kusisimua, vigezo vilivyotumika katika kugawa kipera hiki ni pamoja na lugha inayotumika, lugha inayotumika katika kipera hiki ni lugha ya kishairi, fani iliyotumika ni fani ya kihadithi ambayo ni hadithi fupi, nyepesi na inavisa vya kusisimua na kigezo kingine ni muktadha wa uwasilishaji ambapo huimbwa au kughanwa ikiambatana na ala za muziki.
Ngano; hizi ni hadithi za mapokeo zitumiazo wahusika kama wanyama, miti na watu katika kuelezea au kuonya kuhusu maisha. Katika kipera hiki kigezo kilichotumika ni muktadha wa uwasilishaji, kwamba huwasilishwa pamoja na ala ya muziki. Ngano huwa ghani masimulizi inapowasilishwa pamoja na ala ya muziki.
Sifo; hizi ni tungo za kusifu, kigezo kilichotumika ni muktadha wa uwasilishaji: sifo huwa ghani masimulizi inapoingiza muziki katika utondozi wake, lugha iliyotumika ni lugha ya kishairi.
Tendi; hizi ni ghani ndefu za masimulizi juu ya matendo ya mashujaa yenye uzito kijamii au kitaifa. Vigezo vilivyotumika katika kugawa kipera hiki ni fani ambayo ni huhusu matukio muhimu ya kihisitoria au ya kijamii. Kigezo kingine ni muktadha wa uwasilishaji, hutungwa na kuwasilishwa papo kwa papo.
Utanzu mwingine wa Fasihi Simulizi ni utanzu wa mazungumzo. Mazungumzo ni maongozi au maelezo ya mdomo katika lugha ya kawaida juu ya jambo lolote lile. Si kila mazungumzo ni fasihi ili mazungumzo yaitwe fasihi lazima yawe na usanii wa aina fulani. Vigezo vilivyotumika katika kugawa utanzu huu ni kigezo cha lugha ambapo lugha iliyotumika ni lugha ya kifasihi. Kigezo kingine ni kigezo cha kimuundo ambapo muundo wake huwa wa kidayalojia.
Utanzu huu wa mazungumzo una vipera vifuatavyo ambavyo ni hotuba, malumbano ya watani, soga, mawaidha na ulumbi.
Hotuba; haya ni mazungumzo ambayo huwasilishwa kwenye vikao rasmi vya kimila, kisiasa au kidini. Vigezo vilivyotumika katika kugawa kipera hiki ni kigezo cha lugha ambapo lugha yake huwa rasmi, sanifu na ya kisanaa. Kigezo kingine ni kigezo cha kimuktadha ambapo hotuba huwasilishwa katika mazingira maalumu kwa mfano katika vikao rasmi au mikutano.
Malumbano ya watani; haya ni mazungumzo yanayozingatia masharti yanayotawala uhusiano wao wa kiutani. Huweza kuwa utani wa kikabila, utani wa mababu au mabibi na wajukuu. Vigezo vilivyotumika katika ugawaji wa kipera hiki ni kigezo cha lugha ambapo lugha huwa ni ya kimafumbo. Kigezo kingine ni kigezo cha wahusika ambapo wahusika huwa na uhusiano wa karibu.
Soga; haya ni mazungumzo ya kupitisha wakati ili kusubiri kitu fulani. Vigezo vilivyotumika katika kugawa kipera hiki ni kigezo cha kidhima ambapo dhima yake ni kupitisha wakati. Kigezo kingine ni kigezo cha lugha ambapo lugha inayotumika siyo rasmi. Vilele kuna kigezo cha muktadha ambapo muktadha wake huwa ni mahali popote.
Mawaidha; haya ni maneno ya maonyo au mafunzo aghalabu huwa ya kidini na yenye muongozo. Kigezo kilichotumika katika kugawa kipera hiki ni kigezo cha kidhima ambapo dhima yake ni kuonya au kutoa muongozo.
Ulumbi; huu ni uhodari wa kuzungumza ambao huwa ni wa kiufasaha na madoido. Vigezo vilivyotumika katika kugawa kipera hiki ni kigezo cha kifani ambapo lugha iliyotumika ni lugha ya kimadoido na kifasaha.
Utanzu mwingine katika Fasihi Simulizi ni utanzu wa maigizo. Maigizo ni michezo ambayo hutumia watendaji wa kuiga tabia na matendo ya watu au viumbe wengine ili kuburudisha na kutoa ujumbe fulani kwa hadhira. Vigezo vilivyotumika katika kutenga utanzu huu ni kigezo cha namna ya uwasilishaji ambapo huwasilishwa kwa kuiga matendo ya watu au wanyama. Kigezo cha kidhima ambapo dhima yake ni kuburudisha, kuelimisha au kuonya. Pia kimetumika kigezo cha mandhari ambapo maigizo huambatana na matukio maalumu kama vile kwenye maadhimisho ya sherehe fulani na katika matukio ya kijamii.
Utanzu mwingine wa Fasihi Simulizi ni utanzu wa ngomezi. Ngomezi ni ile hali ya kupeleka ujumbe kwa kutumia mdundo wa ngoma. Vigezo vilivyotumika katika utanzu huu ni kigezo cha kifaa cha uwasilishaji ambacho ni ngoma. Pia kigezo kingine ni kigezo cha kidhima ambapo dhima yake ni kupeleka taarifa fulani kwa jamii. Mfano taarifa hiyo yaweza kuwa ya msiba, mkutano na kadhalika.
Pamoja na ugawaji huu wa tanzu na vipera vya Fasihi Simulizi uliofanywa na Mulokozi kwa kuzingatia vigezo vyake alivyovitumia, bado ugawaji huu unaudhaifu mkubwa tu. Udhaifu au changamoto za vigezo alivyovitumia Mulokozi ni kama ifuatavyo:-
Vigezo vyote hivi vinaweza kuingiliana; mfano kigezo cha kidhima, kama vile kuonya au kuelimisha huweza kuonekana katika tanzu zaidi ya moja au hata katika vipera mbalimbali.
Pia kigezo cha namna ya uwasilishaji huweza kuingiliana kutoka utanzu mmoja hadi mwingine. Mfano, katika utanzu wa masimulizi na mazungumzo.
Vilevile kigezo cha wahusika; kigezo hiki huweza kuingiliana katika utanzu mmoja na mwingine. Mfano, unaweza kuwa na hadithi yenye wanyama, binadamu, mizimu na kadhalika. Hivyo inakuwa si jambo rahisi kuona tofauti zilizopo.  
Kwa kuhitimisha, tunaweza kusema kwamba ni vigumu kuainisha tanzu na vipera vya Fasihi Simulizi kutokana na kwamba, Fasihi Simulizi hubadilika badilika kifani, kimaumbo na hata kimaudhui kwa kutegemea muktadha na namna ya uwasilishaji wake. Kwa mfano ngano iliyopo katika masimulizi ni tofauti na ngano iliyopo katika maghani. Hivyo basi tatizo hili linaweza kutatuliwa kwa kutumia istilahi tofauti katika vipera au tanzu zinazoingiliana.         
MAREJEO:
Mulokozi, M. M. (1989). Tanzu za Fasihi Simulizi: Katika Mulika 21. TUKI. Dar es Salaam.
Mulokozi, M.M. (1996). Utangulizi wa Fasihi Simulizi ya Kiswahili. TUKI. Dar es Salaam.
Wamitila, K.W. (2003). Kamusi ya Fasihi, Istilahi na Nadharia. Focus Publications Ltd.                                                       Nairobi.
TUKI, (2004). Kamusi ya Kiswahili Sanifu. (Toleo la Pili). East Africa: Oxford University Press na Taasisi ya Uchunguzi wa Kiswahili (TUKI).